Select Menu

Ads

Random Posts

Powered by Blogger.

Design

Technology

Circle Gallery

Shooting

Racing

News

Bottom

Thursday, July 17, 2014

Matokeo kidato cha sita yatia fora

Dar es Salaam. Baraza la Mitihani la Taifa (Necta) limetangaza matokeo ya kidato cha sita kwa mwaka 2014 ambayo yanaonyesha kupanda kwa kiasi kikubwa cha ufaulu kutoka asilimia 87.85 mwaka 2013 na hadi 95.98 mwaka huu. 
Kaimu Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa (Necta) Dk Charles E. Msonde

Katika matokeo hayo yaliyotangazwa jana na Necta, orodha ya kumi bora imetawaliwa na shule nyingi zenye majina yasiyo maarufu, huku shule maarufu ya sekondari ya Tambaza na ya Ufundi ya Iyunga zikiwa miongoni mwa shule 10 zilizoshika mkia. 
Matokeo ya Kidato cha Sita 2014 (ACSEE 2014) yapo hapa

Hata hivyo, ufaulu wa mwaka huu unaonekana kuchangiwa na idadi ndogo ya watahiniwa kulinganisha na mwaka jana, hali ambayo imejionyesha pia kwenye idadi ya wanafunzi waliohusika na udanganyifu ambao mwaka huu ni wawili tofauti na wanne wa mwaka jana.

Baraza la Mitihani la Tanzania linapenda kutumia fursa hii kuzipongeza Kamati za Uendeshaji Mitihani za Mikoa na Wilaya, wakuu wa shule na wasimamizi wa mtihani uliofanyika Mei, 2014 kwa kuzingatia na kusimamia taratibu za uendeshaji mitihani na hivyo kuzuia udanganyifu kufanyika,” alisema kaimu katibu mtendaji wa Necta, Dk Charles E. Msonde wakati alipozungumza na waandishi wa habari jana. 

Aidha Baraza linawapongeza watahiniwa wote waliofanya mtihani wa kidato cha sita 2014 kwa kutojihusisha na udanganyifu,” aliongeza katibu huyo ambaye alijikita katika taarifa aliyoiandaa kutangaza matokeo hayo. 

Mwaka huu waliofanya mtihani walikuwa 40,695 na waliofaulu ni 38,905 ambao ni sawa na asilimia 95.98, wakati mwaka 2013 watahiniwa waliofanya mtihani walikuwa 50,611 na waliofaulu walikuwa 44,366 sawa na asilimia 87.85.

Katika matokeo hayo, wavulana wameendelea kufanya vizuri katika masomo ya sayansi huku wasichana wakifanya vyema katika masomo ya lugha na biashara.  Dk Msonde alisema ufaulu wa mitihani umeimarika ikilinganishwa na miaka ya nyuma. 
Watahiniwa wa shule, kati ya 35,650 waliosajiliwa ni 35,418, sawa na asilimia 99.35, walifanya mtihani. Wasichana walikuwa 11,022 sawa na asilimia 99.63 na wavulana walikuwa 24,396, sawa na asilimia 99.22. 
Dk Msonde alisema watahiniwa wa kujitegemea waliosajiliwa walikuwa 6,318. Kati yao, watahiniwa 5,277 (asilimia 83.52) walifanya mtihani na watahiniwa 1,041 (asilimia 16.48) hawakufanya mtihani. 

Jumla ya wasichana waliofaulu ni 12,080 sawa na asilimia 97.66 wakati wavulana ni 26,825 sawa na asilimia 95.25 ya watahiniwa wote 38,905 waliofanya mtihani,” alisema Dk Msonde. 
Ubora wa ufaulu kwa kuangalia madaraja waliyopata watahiniwa wa shule unaonyesha jumla ya watahiniwa 30,225 sawa na asilimia 85.73 wamefaulu katika madaraja I-III wakiwamo wasichana 9,954 sawa na asilimia 90.59 na wavulana 20,271 sawa na asilimia 83.53.”

Kuhusu matokeo yaliyozuiwa, Dk Msonde alisema matokeo ya watahiniwa 150 yamezuiwa kwa sababu hawajakamilisha ada ya mtihani hadi watakapolipa.  Alisema watahiniwa tisa walipata matatizo ya kiafya wakati wakiendelea na mitihani na 29 hawakufanya kabisa kwa sababu hizo za kiafya na wamepewa fursa ya kufanya mitihani Mei mwakani. 
Baraza limefuta matokeo yote kwa watahiniwa wawili waliobainika kufanya udanganyifu katika mitihani,” alisema Dk Msonde. 
Mwaka jana watahiniwa wanne walifutiwa matokeo yote kwa kufanya udanganyifu ndani ya chumba cha mitihani.

Alisema pia kuwa, mfumo wa upangaji wa shule bora kitaifa umebadilishwa na kuwa kundi moja. Awali zilitengwa makundi mawili ya watahiniwa zaidi ya 30 na chini ya 30 sasa yameunganishwa pamoja. Pia upangaji wa watahiniwa waliofanya vizuri umefanyiwa mabadiliko, awali ilikuwa wanafunzi watano waliofanya vyema masomo ya sayansi, biashara na lugha lakini mwaka huu wameongezeka na kuwa 10 kwa kila kundi. 
Dk Msonde alisema mtahiniwa alihesabiwa kuwa amefaulu angalau awe amepata gredi D (alama 30) kwa somo husika huku kiwango cha juu cha ufaulu kilikuwa gredi A.

Mpangilio wa alama  

Dk Msonde alisema pia kuwa alama A ilianzia 75-100, B+ ni 60-74, B 50-59 wakati C 40-49. Alama nyingine ni D 30-39, E 20-29 na F 0-19. 
“Daraja la I lilianzia pointi 3-7, II 8-9, III 10-13, IV na mshindi angalau anatakiwa awe na angalau D mbili au ‘Principal Pass’ moja isiyopungua C na 0 aliyepata ufaulu chini ya D mbili.  Shule 10 bora kitaifa  Dk Msonde alizitangaza shule kumi bora kitaifa kuwa ni Igowole (Iringa), Feza Boys (Dar es Salaam),
Kisimiri (Arusha), Iwawa (Njombe), Kibaha (Pwani), Marian Girls (Pwani), Nangwa (Manyara), Uwata (Mbeya), Kibondo (Kigoma) na Kawawa (Iringa). 

Shule 10 za mwisho kitaifa


Kaimu Katibu Mtendaji huyo alizitaja shule hizo kuwa ni: Ben Bella (Unguja), Fidel Castro (Pemba), Tambaza (Dar es Salaam), Muheza (Tanga), Mazizini (Unguja), Mtwara Technical (Mtwara), Iyunga Technical (Mbeya), Al-Falaah Muslim (Unguja), Kaliua (Tabora) na Osward Mang’ombe (Mara). 

10 bora masomo ya Sayansi  

Tofauti na miaka ya nyuma Necta imepanga watahiniwa waliofanya vizuri katika makundi matatu ambayo ni sayansi, biashara na lugha.

Watahiniwa waliofanya vizuri kwa masomo ya sayansi kitaifa na shule na mkoa katika mabano ni: Isaack Shayo (St. Joseph Cathedral-Dar es Salaam), Doris Noah (Marian Girls-Pwani), Innocent Yusufu (Feza Boys-Dar es Salaam), Placid Pius (Moshi-Kilimanjaro) na Benni Shayo (Ilboru-Arusha). 
Wengine ni: Abubakar Juma (Mzumbe-Morogoro), Mwaminimungu Christopher (Tabora Boys- Tabora), Chigulu Japhaly (Mzumbe Morogoro), Hussein Parpia (Al-Muntazir Islamic Seminary-Dar es Salaam) na Ramadhani Msangi (Feza Boys-Dar es Salaam.)

10 bora masomo ya Biashara  

Jovina Leonidas (Ngaza-Mwanza), Nestory Makendi (Kibaha-Pwani), Imma Anyandwile (Umbwe- Kilimanjaro), Theresia Marwa na Grace Chelele wote kutoka Loyola- Dar es Salaam.  Wengine ni Betrida Rugila (Baobab- Pwani), Jacqueline Kalinga (Weruweru- Kilimanjaro), Tajiel Kitojo (Arusha- Arusha), Shriya Ramaiya (Shaaban Robert-Dar es Salaam) na Manaid Mwazema.  10 bora masomo ya Lugha 
Lisa Mimbi (St. Mary Goreti- Kilimanjaro), Rosalyn Tandau (Marian Girls- Pwani), Joseph Ngobya (St. Joseph Cathedral- Dar es Salaam), Aneth Mtenga na Idda Lawenja kutoka Marian Girls- Pwani. 
Wengine ni Edna Mwankenja (Kisimiri-Arusha), Catherine Kiiza (St. Mary’s Mazinde Juu- Tanga), Nancy Swai (Mwika-Kilimanjaro), Mohamed Salmin (Mwanza-Mwanza) na Idrisa Hamisi (Mwembetogwa-Iringa).